Wednesday, January 29, 2020

DEFEND YOUR FAITH AS A CATHOLIC: Maisha ni sasa

DEFEND YOUR FAITH AS A CATHOLIC: Maisha ni sasa: Napenda kuanza kwa kusema kuwa ‘The means justify the end.’ Nikimaanisha namna ya maisha yetu ya sasa ndiyo yanayo au yatakayotuwezesha ku...

DEFEND YOUR FAITH AS A CATHOLIC: KIFO

DEFEND YOUR FAITH AS A CATHOLIC: KIFO:  Sababu zinazoweza kupelekea Kifo [1] Kila mmoja wetu amekwisha kutambua ya kuwa kifo ni lazima tukipitie. Kwa kuwa hata katika uumbaji ...

DEFEND YOUR FAITH AS A CATHOLIC: AMRI ZA KANISA

DEFEND YOUR FAITH AS A CATHOLIC: AMRI ZA KANISA:                                          Amri za Kanisa Kuna jumla ya amri sita za Kanisa. “Amri hizi za Kanisa zimepangwa katika fumo ...

AMRI ZA KANISA


                                         Amri za Kanisa

Kuna jumla ya amri sita za Kanisa. “Amri hizi za Kanisa zimepangwa katika fumo wa maisha ya maadili, zikifungamanishwa na kulishwa na maisha ya Liturujia. Sheria hizi zilizowekwa wazi na mamlaka ya kichungaji zina hali faradhi kwa lengo la kuwathibitishia waamini kiwango cha chini kabisa cha lazima katika roho ya sala na juhudi ya maadili, katika kukua katika mapendo kwa Mungu na jirani.”[1]  Nazo ni zifuatazo kulingana na Misale ya waumini:[2]
1.  Hudhuria Misa Takatifu Dominika na sikukuu zilizoamriwa.
Inamtaka mwamini kutakatifuza siku ya kumbukumbu ua fumbo la Ufufuko wa Bwana, lakini pia sikukuu kubwa za kuheshimu mafumbo ya Bwana, ya Bikira Maria Mwenye heri, na ya Watakatifu. Kwanza, kwa kushiriki adhimisho la Ekaristi ambamo jumuiya ya Kikristo inakusanyika, na kupumzika na kuacha zile kazi na shughuli ambazo kwayo zingezuia kutakatifuza siku hizo.[3]  Lakini pia mwamini apumzike kwa kuacha kazi nzito.[4]
2.  Funga siku ya jumatano ya majivu; usile nyama siku ya Ijumaa Kuu.
Ndugu yangu unayesoma kitabu hiki, unapoongelea Jumatano ya Majivu huwezi kutupilia mbali Kwaresima, maana Jumatano ya Majivu ndiyo mlanngo wa kutuingiza katika Kwaresima. Kumbe hatuna Kwaresima pasipo Jumtano ya Majivu. Siku ya Jumatano ya Majivu tunaanza rasmi kipindi cha Kwaresma ambacho kinadumu kwa muda wa siku arobaini. Kwa nini siku arobaini? Waisraeli walikaa jangwani sku arobaini, gharika kuu ilidumu siku arobaini, Yesu alifunga siku arobaini, kwaresma inadumu siku arobaini. Miaka/siku arobaini katika Maandiko matakatifu inawakilisha kipindi kamili cha mpito ambacho ndanimo jambo linaweza kufanyika na likakamilika. Hivyo Kwaresma ni kipindi kamili cha mpito ambacho ndanimo mapinduzi ya kiroho yanaweza kufanyika. Ni kipindi cha kufanya maandalizi ya kuadhimisha sikukuu ya Pasaka.  Na hivyo kinaambatana na kupakwa majivu yatokanayo na matawi tuliyotumia Dominika ya matawi; katika paji la uso kwa waamini lakini kwa Waklero kichwani. Katika kipindi hiki mama Kanisa anatualika kufanya tathimini ya mahusiano yetu na Mungu. Ni kipindi cha kufanya mapinduzi ya kiroho.Waamini tunahimizwa kwa naamna ya pekee kuhudhuria liturjia ya leo.[5] Majivu tutakayopakwa ni alama ya ukubali wetu kwamba sisi ni wadhambi, hatuna thamani mbele ya Mungu na tunahitaji kufanya toba.

Katika ulimwengu wa wayahudi majivu yalikuwa ni alama ya huzuni, masumbuko, uchungu au uduni.[6] Baadaye utamaduni huu wa kupakana majivu ulitumiwa na wakristo wa kwanza kama alama ya toba. Mwaka 600 hivi, Gregory Mkuu aliifanya siku ya Jumatano ya majivu kuwa siku ya kwanza ya Kwaresma na akaongeza urefu wa kipindi hiki cha toba hadi siku arobaini. Miaka ya 800 hivi, baadhi ya makanisa yaliadhimisha ibada ya Jumatano ya majivu kwaajili ya wadhambi waliokubuhu katika dhambi na waliojulikana. Sasa pale walipoamua kufanya toba ndio walipakwa majivu. Hivi wakati huu si wote walipakwa majivu ila tu wale walikuwa wadhambi waliojulikana wazi, kama vile Malaya, wauaji, waasi n.k. Kuanzia karne ya 11, Kanisa lilipanua ibada hii na kuwahusisha waamini wake wote na si wadhambi waliokubuhu tu. Hatua za kuchukua ili tuweze kufanya vema mapinduzi ya kiroho, toba na kubadilika. Tukubali kwamba sisi ni wadhambi. Tusipokubali kuwa sisi ni wadhambi halafu hatutaona hitaji la kufanya toba na kubadilika. Ndio maana tunapakwa majivu ikiwa ni alama ya kukubali kuwa sisi ni wadhambi hatuna thamini mbele ya Mungu, na hivi tunahitaji kutubu. Kutumia misaada mbalimbali ambayo itatusaidia kumrudia Mungu: Sala, kufunga na matendo ya huruma. Na hivyo kwa kutambua tu wadhambi ndiyo maana tunapaswa kufunga siku hiyo ya Jumatano ya majivu.

Lakini pia usile nyama siku ya Ijumaa Kuu. Tukumbuke ndiyo siku Mkombozi wetu Yesu Kristo anakufa msalabani. Na hivyo hatupaswi kula nyama kama waamini wenye kutambua thamani ya wokovu wetu. Kwahiyo, ni siku ambayo waamini wanakuwa katika huzuni, wakiomboleza juu ya kuondokewa na Mpendwa wao. Kama tujuavyo katika hali ya maisha yetu ni kwamba nyama inatumika na kuthaminiwa kama chakula fulani cha hali ya juu, yenye thamani na nzuri sana; ni katika uzuri huo watu wanaona fahari na kuwafanya wafurahie. Mfano mzuri ni huu, ukitaka kuona au kusikia sherehe fulani wanaisifia kuwa ilikuwa nzuri; wengi waseamao utasikia yaani walijipanga kwelikweli: nyama ilikuwa ya kutosha kwa maana walichinjwa labda ng’ombe watano (5) na kitakachofuata ni kinyaji, utasikia kulikuwa na pombe ya kutosha kama ni ya kienyeji au bia au divai n.k. Kwa hiyo, hatunabudi kufunga siku hiyo kula nyama.

3.  Ungama dhambi zako walu mara moja kila mwaka.
Pia sheria hii yahakikisha maandalizi kwa ajili ya Ekaristi kwa kupokea Sakramenti ya Upatanisho.[7] Hii inaonyesha mwendelezo wa kazi ya wongofu na msamaha wa Ubatizo.[8]
4.  Pokea Ekaristi Takatifu hasa wakati wa Paska.
Kama nilivyotangulia kusema, sheria hizi za Kanisa kuwa inatoa walau kiwango cha chini. Kumbe amri hii yahakikisha kiwango cha chini cha kupokea Mwili na Damu ya Bwana kuhusiana na sikukuu za Pasaka, asili na kilele cha Liturujia ya Kikristo.[9] Na hii inaenda sambamba na wale wanaoweza kushiriki Misa zaidi ya moja. Waliowengi hawajui ya kuwa kama umemaliza Misa hii na ukampokea Yesu katika maumbo ya mkate na divai, unapoenda Misa nyingine una haki ya kumpokea tena. Siyo useme tu nimemaliza kumpokea Misa iliyopita na sasa sitaki au siwezi, wewe mpokee labda kama unaona hufai pengine kiroho. Lakini kulingana na mazingira unaruhusiwa kumpokea hata kama unajua kiroho ni mdhambi. Pengine ni kigangoni na Padre amekuja kwa kuchelewa kwa sababu za kichungaji, basi usishindwe kwenda kumpokea ilimradi tu ulikuwa umeshaweka nia ya kuungama kwanza. Na hivyo ukiwa katika nia hiyo unaruhusiwa kukomonika, ila unuie kuwa mara baada ya kukomonika basi unamtafuta Padre kwa maungamo. Ukifanya hivyo utakuwa hujatenda dhambi na katika kumpokea Yesu maadam hujasitahilishwa basi inakuwa siyo kufuru na unakuwa hujajitwalia hukumu yako.  
5.  Saidia Kanisa Katoliki kwa zaka.
Ina maana ya kwamba waamini wana wajibu na kazi ya kusaidia kutoa mahitaji ya Kanisa kila mmoja, kadiri ya uwezo wake.[10] Zaka hii inapaswa kutolewa fungu la kumi la kile unachojaliwa au ulichojaliwa.[11]
6.  Shika sheria Katoliki za ndoa.
Lakini kwanza tutambue kuwa ndoa ni sakramenti kwa wakristo na hasa kwa wakatoliki. Ndoa ni agano kati ya mtu mume na mtu mke. Ndoa ni aganao linalowafanya wanandoa kusihi pamoja kwa maisha yao yote.[12] Kwa kweli nakosa hata nguvu za kuongelea juu ya amri hii. Walio wengi naamini ni mashahidi, ya kwamba amari hii haitendewi haki na wale wenye kuitendea haki. Sina uhakika ni watu wangapi ambapo kwa uwazi kabisa tukiwauliza juu ya amri hii kama wanaijua vilivyo; hususani wanandoa. Mama Kanisa katuwekea sheria jumla mia moja na kumi na moja (111) za ndoa.[13]  Sheria zenyewe hizi zimegawanyika katika sehemu kumi (10) kwa kadiri ya Kitabu cha kanuni ya Kanisa Katoliki toleo la pili la mwaka 1983.
a)  Mtazamo wa kichungaji na nini kinatangulia maadhimisho ya ndoa (Pastoral care and what must proced celebration of marriage)
b)  Vipigamizi vya ndoa kwa ujumla (Diriment impediment in general)
c)   Vipingamizi vya ndoa moja kwa moja (Diriment impediment specifically)
d)  Makubaliano ya ndoa (Matrimonial consent)
e)  Nguvu ya ndoa (Force of marriage)
f)    Ndoa mchanganyiko (Mixed marriage)
g)  Kuadhimisha ndoa wa siri (The secret celebration of marriage)
h)  Athari za ndoa (Effects of marriage)
i)    Kuwatenganisha wanandoa kwa muda (Simple separation of spouses)
j)    Kuhalalisha ndoa ambayo haikuwepo (The convalidation of marriage).[14]




[1] KKK Na. 2041.
[2] Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, Misale ya Waamini, Toleo la Kumi, TMP Book Department, Tabora- Tanzania, 2008, uk. 1077.
[3] Rej. MSK. Na. 1246- 1248.
[4] Rej. KKK Na. 2042.
[5] Rej. Katekisimu ndogo ya Katoliki Jimbo la Iringa, Na .97, 100.
[6] Rej. Ayu 2: 8, 30: 19; Zab 102: 10.
[7] Ibid.
[8] Rej. MSK. Na. 989, 719.
[9] Rej. Sheria za Kanisa Katoliki, CIC Na. 920, 708, 881.
[10] Rej. Sheria za Kanisa Katoliki, CIC Na. 222, 1249-1251, 882, 25.
[11][11] Rej. Law 27:30-33.
[12] Rej. Elias Nada, Karne ya Ishirini na Moja na Ndoa za Kikristo, Sayansi, Maisha ya Familia na Ndoa, Chapa ya pili, Timia Printers, Moshi, 2015, uk. 25.
[13] Rej. Sheria za Kanisa Katoliki za Ndoa, Mada ya saba Ndoa (CIC 1055-1165).
[14] The Code of the Canon Law, New Revisedd English Translation, Harper Collins Publishers, Newsland, 1983, 237-258.
[15] Eze 18:23-28.

Tuesday, January 28, 2020

KIFO


 Sababu zinazoweza kupelekea Kifo[1]

Kila mmoja wetu amekwisha kutambua ya kuwa kifo ni lazima tukipitie. Kwa kuwa hata katika uumbaji (uhulushi) tunajua ya kwamba mwanadamu ni mwili na roho. Mara tu baada ya kutungwa kwa mimba, basi Mungu mwenyewe ndiye aiwekaye roho hiyo. Mwili daima unakufa, lakini roho kamwe haifi. Ndiyo maana mtu baada ya kufa mwili ule unaoza kwani umeumbwa kwa kitufaa (matter or material). Kwa lugha nyingine ni kwamba; ‘material body or things normally corruptible, hence decay’.[2] Kwani kupitia kuonja mauti, ndiyo njia pia itupasayo kufika kwa Baba. Huko ndipo tutaenda kuishi na kustarehe kwa umilele. Sasa kwa kuwa kifo ni matokeo ya dhambi ya asili waliyoifanya wazazi wetu wa kwanza yaani Adamu na Eva. Zifuatazo zinaweza zikawa sababu ambazo zinaweza kupelekea kifo, kwa kila mmoja wetu. Japo ni fumbo kwetu kama wanadamu kutambua tutakipitia kifo kwa njia ipi. Ila uhakika tulionao tu ni kwamba lazima kifo tukipitie.

1 Magonjwa

Kama tutambuavyo mapisi (historia) ya Adamu na Eva kule bustanini, ya kuwa waliishi vizuri na wanyama tena. Lakini baada ya kukosa utii, Mungu aliamua kuwafukuza bustanini na kuwapa mapigo kadhaa. Kama tutambuavyo ya kuwa hata dhahabu hujaribiwa kwa moto, ndivyo hivyo nasi tunakutana na magonjwa mbalimbali ili kuyafanya maisha yaende cha mikikimikiki. Kwa hiyo, maisha yetu kutokana na waandami (watangulizi) yaani wazazi wetu wa kwanza, nasi hatunabudi kuyapokea mahangaiko, mateso yatokanayo na maradhi. Kwani ardhi yote imelaaniwa kwa sababu wazazi wetu, vivyo hivyo nasi tunapatwa na yale aliyosema Mungu kama laana juu yetu.
Sasa katika maisha yetu tunaona na kushuhudia watu wengi wakifa kwa sababu mbalimbali za magonjwa. Na kinachosikitisha zaidi ni kwamba wakati huu watu wamekuwa wengi na magonjwa nayo yameongezeka sana. Kuna magonjwa ya aina mbalimbali ila zaidi ni ya kuambukizwa na yale yasiyoyambukizwa. Lakini yote katika yote unachelewa kupata huduma basi ugonjwa ukawa umeshamaliza au umeshatawala mwili kwa kiasi kikubwa basi hata matibabu unayowekupata yanaweza tu kukusaidia kusogeza siku au hata masaa. Magonjwa ambayo ni tishio sana kwetu mpaka sasa ni Mgandamizo wa damu (Presha), kisukari, ugonjwa wa moyo, saratani au kansa, UKIMWI pia malaria. Haya kwa kiasi kikubwa yamekuwa changamoto sana siku hizi. Mbaya zaidi yaliyomengi yanayoonekana kuwa kama tishio kwa kipindi hiki, mengi yanachangiwa na matumizi ya vyakula. Tunajikuta tumelalia kula vyakula vya kisasa (vyakula vinavyopita viwandani) zaidi kuliko vile vya asili. Vyakula vilivyojaa sana mafuta.
Tahadhari ni kwamba watu waanze kuwa na mazoea ya kupima na kuchunguza afya zao mara kwa mara ili kujua maendeleo ya afya zao. Hii isifanyike kwa ratiba bali iwe kila mara unapopata nafasi ya kufanya hivyo basi fanya. Kwani unapogundulika unatatizo fulani na ukawa tayari kufuata maelekezo ya Madaktari, aidha kwa kuacha kula aina fulani za vyakula au kwa kula aina fulani tu za vyakula basi utakuwa katika nafasi nzuri ya kuuweka mwili wako katika mazingira safi ya kupamabana na maradhi mengine ambayo yanaweza kujitokeza.
Lakini pia kuna maradhi mengine sisi wenyewe tumekuwa chanzo cha kuyasababisha. Kwa mfano kuna magonjwa ya mripuko ambayo unakuta chanzo chake kikuu ni kushindwa kutunza mazingira yetu salama. Hali tukitambua kuwa tukiyatunza mazingira hakika nayo pia yatatutunza. Kwa mfano kuna watu wanakufa kwa sababu ya mripuko wa ugonjwa wa Kipindupindu au Ebola. Sasa mtu watu hawa waathirika wanapokosa msaada wa huduma ya haraka lazima tuwapoteze, maana hamna namna. Kwa hiyo, tuwe makini na tutunze mazingira yetu nayo yatatutunza na kutuweka salama.

2 Ajali

Si kila ajali inatokea kwa sababu ya uzembe wa wale wenye dhamana ya kuongoza vyombo hivyo vya safari. Lakini zilizo nyingi chanzo kikubwa ni uzembe wa wahusika. Kuna aina mbalimbali za usafiri ukiwemo wa nchi kavu (Barabarani), majini pia angani. Sasa mara nyingi utakuta ni uzembe wa Dreva ama Nahodha ama Lubani kushindwa kuwa makini wakati anaongoza chombo. Na hii inatokana na kuwa na mawazo tawanyishi. Yaani mawazo yake muda fulani yanakuwa yametawanyika, badala ya kuwaza kile chombo anachoongoza anawaza yaliyo nje ya pale. Sasa hali hiyo inapoendelea inaweza kumfanya apoteze mwelekeo. Apotezapo mwelekeo tu, maana yake anaposhindwa kufuata vigezo na masharti ya uongozaji basi utasikia ajali imetokea.
Si hivyo tu, bali wakati mwingine inatokana na uchakavu wa vifaa au vimbo hivyo. Yaani unakuta ni chombo cha usafiri na kila siku au kila mara kiko safarini, kwa bahati mbaya uangalizi unapokuwa hafifu au mdogo. Sasa kama hamna uangalizi (kufanya service), kuna siku kinaweza kuwa kibovu na kwa kuwa hakina uangalizi wa mara kwa mara au kabla ya kuanza safari; basi mwisho wa siku kikiwa safarini na tatizo limeshakuwa kubwa utasikia kimepata ajali na watu kadhaa wamefariki dunia papo hapo na wengine kadhaa wamejeruhiwa. Kwa hiyo, kuwa na muda wa kuwa tunavihakiki ubora wake ni muhimu sana.
Mara nyingine pia mazingira ya hali ya hewa yanaweza kusababisha ajali. Kuna wakati hali ya hewa ndani ya maji inachafuka yaani unakuta mawimbi yameongezeka na chombo kiko safarini au chombo kiko angani na huko kinakutana na kani ya mvutano na hivyo kupelekea chombo hicho kupoteza mwelekeo. Hatimaye kinashindwa kumudu au kukabiliana na hali hiyo, basi kinabaki kuongozwa na hali ya hewa ya wakati huo. Na baadaye utasikia kimepata ajali. Kama tujuavyo Meli ya Mv. Bukoba ilivyozama tarehe 21-05-1996 na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 800.
Lakini pia sababu nyingine ya ajali inakuwa ni Dreva mwenyewe asiyejali mwendokasi. Mfano ulio hai ni huu, kuna aina tatu za Madreva; Dreva Kenge (huyu ni Dreva wa kukurupuka, pasipo kujali ubora wa chombo chake pia mwendokasi), Dreva Nyoka (huyu anaendesha kwa kupindapinda, yaani anaenda kwa kukatakata makona mfano anataka kumpita mwenzake shemu mbaya au isiyoruhusiwa na akiwa katika mwendokasi), na wa mwisho ni Dreva Kinyonga (huyu ni Dreva anayeendesha kwa usalama na anafuata kanuni zote za barabarani vizuri). Kumbe mwendokasi unapelekea wakati mwingi ajali, maana anapokutana na kona kali na yuko mwendokasi lazima limshinde kukata kona, mwisho wa siku gari litamshinda kumtawala na kuanguka au kupindukapinduka.
Ajali nyingine zinakuwa za mtu husika mwenyewe. Pengine ni fundi umeme. Sasa akiwa yuko juu ya nguzo akateleza na kuanguka, kwa bahati mbaya akaangukia sehemu mbaya. Kumbe inaweza kumpelekea katika kifo. Wakati mwingine watoto wanapenda kukwea juu ya miti yenye matunda misimu yake ikifika. Sasa inatokea wakati fulani akiwa amekwea anakanyaga tawi vibaya au tawi alilokanyaga bila kujua likawa limeshakauka. Mwisho wa siku anajikuta ameshashuka nalo chini. Na pengine mazingira ya pale chini yakawa hayako vizuri, basi anapoanguka vibaya basi inaweza kumpelekea katika kifo.

3 Vita

Kinyume cha vita ni amani. Kwa hiyo, kwa maneno mengine vita ni ukosefu wa amani. Kumbe vita inaambatana na utumiaji wa nguvu kupita kiasi (yaani silaha). Vita kwa yenyewe siyo kitu kizuri, kwani mara zote inaenda sambamba na umwagaji wa damu kwa watu wasio na hatia au wenye hatia. Licha ya kwamba katika maadili inaongelea katika sababu yenye haki, basi kwa haja ya hali ya kujihami n akujilinda basi itumike. Lakini katika yote, licha ya sababu inayotambulika hata kimaadili. Bado vita lazima ihusishe mauaji. Kwa mfano wa vita ya kwanza ya dunia mwaka 1918, pia tazama mauaji ya kimbari (Mauaji dhidi ya Wtutsi) kule Rwandwa kati ya 7-04 mpaka 15-07 mwaka 1994. Sasa takribani watu 500,000 mpaka 1,000,000 waliuawa. Kati yao asilimia 70 wakiwa Watutsi;[3] vita zote hizi zilihusisha mauaji ya watu wengi sana. Tusiende mbali sana hata  kwetu tukikumbuka vita ya Tanzania na Uganda (Vita vya Kagera) dhidi ya Idi Amin Dada iliyodumu kwa muda miezi sita, kuanzia mwaka 1978 mpaka 1979. Inasadikika takribani Askari wa Tanzania 373, Raia pia takribani 1500 na Askari 600 miongoni mwa 3000 wa Libya nao waliuawa.[4] Ilihusisha vifo vya watu wengi tu. Na katika hao wapo waliokuwa hawana hatia lakini wengine walikuwa ni wenye hatia.

4 Mamlaka

Katika nchi basi serikali imetoa dhamana kwa chombo fulani kushughulikia mambo kama hayo ya utoaji wa uhai. Kwa mfano nchi ya  Tanzania imetoa mamlaka katika vyombo viwili kwa wale wanobainika kuwa waharifu. Kuna chombo cha Mahakama, ambayo ndiyo inayotoa hukumu kwa watu wanaobainika kufanya makosa makubwa. Lakini utekelezaji wa agizo la mahakama unafanya na chombo cha Magereza. Kumbe, pale mtuhumiwa anapokuwa amehukumiwa kifo yaani kunyongwa na mahakama; ni jukumu la Magereza kuteke agizo hilo kwa mujibu wa mamlaka waliyonayo. Sasa utekelezaji wa mamlaka huo unapofanyika, basi hupelekea kifo kwa mtuhumiwa.

5 Kujitoa mhanga

Tumekuwa tukisikia mashambulio mbalimbali yanayotekelezwa na vikundi mbalimbali katika nchi fulani. Mashambulio haya ndiyo kusema kwa lugha nyingine ugaidi.  Utekelezaji wa kujitoa mhanga huu unawezakunywa na mtu mmoja, kwa kutumia silaha za miripuko; ambapo anatekeleza shambulio hilo la kujitoa mhanga akiwa katika mazingira ya kuzungukwa na watu wengi. Ni dhamiri ya kuwa kwa kutenda hivyo anajikuta kajiua na kuwaua wengine wengine. Kwa mfano tumekuwa tukisikia vikundi kama Alshababu kule Nchini Somalia, Boko haram kule Nchini Nigeria, Alkaida na vingine vingi. Ambavyo mara kadhaa vimekuwa vikiripotiwa kufanya mashambulizi ya kujitoa mhanga katika njia kadhaa. Kumbe kwa kitendo cha kujitoa mhanga tayari kinaambatana na mauaji ya watu.

6 Umri mkubwa

Hiki ni kifo cha asili (natural death). Kama tujuavyo kuwa uhai tumepewa na Mungu na unatoka kwa Mungu. Vivyo hivyo na maisha yetu yote yako kwa Mungu, kwani ndiye ajuaye ni katika umri gani basi tutapaswa kuyiacha dunia hii. Kwa hiyo, siyo wote walioandikiwa kufikia uzeeni, bali wale wachache. Sasa unapokutana na Mzee kabisa  aliyekula chumvi ya kutosha, yaani aliyefikia hatua ya kulelewa kama mtoto maana hajiwezi kwa lolote. Basi anapokufa tunaona kuwa ni kama haki yake, kwani umri wenyewe unaruhusu. Na watu wa namna hii mara nyingi huwa wanakufa wakiwa usingizini. Yaani kabla ya kulala mmeagana vizuri na hakuwa na tatizo au ugonjwa, ila asubuhi mnaamka kwenda kumjulia hali mnakuta ameshakufa. Kumbe umri unapokuwa wa kutosha basi mwisho wa siku zile seli nazo zinachoka mpaka kufikia hatua ya kutojiweza, hatimaye kupelekea kifo.

7 Majanga ya asili

Majanga ya asili wakati mwingine tunajitafutia vifo kupitia yenyewe aidha kwa kutokujua au kwa kujua. Kwa mfano mtu anaamua kwenda kujenga bondeni ambapo anajua mafuriko yakitokea hawezi kubaki salama, lakini anapoambiwa na kutahadharishwa ya kuwa anapaswa ahame ila yeye anabakia huko. Yakumkuta yakifika licha ya kuwa ni majanga ya asili lakini yeye kajiweka katika mazingira ya kukumbwa na matatizo. Kuna majanga ya kumbunga, tetemeko la ardhi, Tsunami, njaa, ukame pia miripuko ya Volkano. Haya yote ni baadhi ya majanga ya asili, hivyo yanapotokea kwa hakika hayawaachi watu salama. Kuna baadhi wanaenda nayo, yaani kifo kinawakabili. Hatuwezi kuyaepuka kwa kweli zaidi tunaaswa tu kuchukua tahadhari. Kwa mfano tetemeko la ardhi lililotokea mkoa wa Kagera mwaka 2017 lilisababisha maafa makubwa, watu kupoteza nyumba zao na mali zao pia wengine walipoteza maisha (walikufa).

8 Kifo cha maamuzi binafsi

kuna watu tumekuwa tukiwaona au kusikia au hata kushuhudia wakipoteza maisha aidha kwa kujitakia au kwa kutojitakia. Wale wanaojitakia ni kama wale wanaofikia hatua ya kukata tamaa ya kuishi, na mwisho wa siku wanaamua kuchukua uamuzi aliouchukua Yuda Iskalioti wa kujiua kwa kujinyonga. Sasa watu wa hivi mimi nawatazama katika mwono huo, ya kuwa wamejitakia. Lakini kuna wale wanakufa bila kujitakia. Kwa mfano unasikia mambo ya utoaji mimba ambao ni dhahiri ni kuuwa tu. Au mwingine anajifungua vizuri mtoto lakini mwisho wa siku anaamua kumtupa chooni au kichakani. Hicho nacho ni kifo cha mtu asiye na hatia na hakujitakia.



[1] Rej. Richard A. Kungi, Kupata nguvu Saa ya Majonzi, Maana na Uponyaji katika Kifo cha Umpendaye, FGD Tanzania Limited, Dar es salaam, 2018, uk. 4-12.
[2] Ludwig OTT, Fundamentals of Catholic Dogma, J. C. Bastible (ed), P. Lynch (trans.), Tan books and Publishers, Inc, Rockford, 1960, uk. 96-100.
[3] WIKIPEDIA- Rwanda genocide, https://en.m.wikipedia.org/wiki/Rwanda-genocide, retrived on 12/05/2019.

Wednesday, January 22, 2020

Maisha ni sasa


Napenda kuanza kwa kusema kuwa ‘The means justify the end.’ Nikimaanisha namna ya maisha yetu ya sasa ndiyo yanayo au yatakayotuwezesha kuiona ya kesho. Maneno mengine, ni kwamba maisha tuishiyo leo ndiyo yanayotabiri kesho yako wewe, mimi na yule. Kwa hiyo namna ya kuishi kwetu leo, inatupatia fursa ya maandalizi ya maisha ya hapo baadaye mara baada ya maisha ya hapa dunia. Kwa mantiki hiyo, tuna kila sababu ya kujitahidi kuishi maisha ya kulenga hapo baadaye itakuwaje. Kufikiri zaidi (foresee or aim high) itakuwaje, na kama umeshaanza kuishi kwa kuona na kutenda kwa kuangalia au kulenga juu ya mwisho wako ni vizuri.

Endelea na kasi hiyo, kwa kusonga mbele na usirudi nyuma kamwe (Ever forward never backward). Kama mwaliko wa siku zote wa Mheshimiwa Rais Dr. John Joseph Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mara zote anavyopenda kutuasa kama wananchi kuwa tusibaki kutazamana tu bali anasema “Wewe chapa kazi tu.
Pia tukiongozwa na methali isemayo, ‘Ngojangoja yaumiza matumbo’ tuchangamkie fursa kwani wakati wenyewe ndiyo huu wa kufanya na kuandaa maisha yetu ya hapo baadaye kuwa mazuri. Tusikae tukabweteka mpaka kufikia wakati ule wa NINGE…. Ninge…. Hii huja mwisho wa safari, ambapo tunakuwa tumeshachelewa na haiwezekani tena. Kama tusemavyo kuwa ‘maji yakishamwagika huwa hayazoleki.’ Ni kwa mantiki hiyo hiyo tunaona mfano ule wa mtu tajiri na Lazaro. Tajiri anvyomlilia Ibrahimu kwa kumwomba amtume basi aende duniani ili awambie juu ya hali aliyokuwa akipitia ili basi nao wasiweze kuingia huko. Lakini tunaambiwa kati yao wametenganishwa na shimo kubwa, na hivyo haiwezekani. Kwa kuwa kuna wengine walioko huko dunia basi wasipowasikiliza hao nao pia wataingia kwa tajiri alipokuwa. Hapa anatufundisha kuwa haiwezekani tena kurudi nyuma, na hivyo tusiisubirie hiyo ninge….tukajikuta tumeshachelewa sana.[1] Kumbe kwa kuwa mimi na wewe bado tuna nafasi ya kujirekebisha basi tufanye hivyo; kabla ya NINGE… haijaja kusikika masikioni mwetu maana muda utakuwa umeshaisha tena wa kusema tunaweza kurekebisha maisha yetu.
Na hivyo kama wasemavyo kuwa ‘Bahati ya mwenzio usiilalie mlango wazi.’ Kuna mtu mwingine anapenda kuyafanya maisha yake kuwa ya mazoea. Tafadhali, mwanadamu daima ni mwili na roho pia mwanadamu hulka yake ni kubadilikabadilika kama kinyonga. Kubadilikabadilika huku ni kule kutoka hali hasi na kwenda hali chanya. Mfano mtu ameshauriwa kuuacha mwenendowake mbaya na afanye hivyo kweli kwa kubadilika au kubadilisha mwenendo wake. Si hivyo tu, ni busara ya kawaida kwamba unapoenda sehemu ukawakuta wanaomboleza basi nawe jiunge nao katika maombolezo hayo. Na kwa kufanya hivyo kile kinachofanyika pale ni kwa manufaa ya jamii nzima, wala siyo cha mtu binafsi.
Sasa, kuna watu wengine kupitia mazoea tunashindwa kuelewa somo hilo juu ya mabadiliko. Kwa mfano, kuna mtu anamchukulia mtu fulani kuwa wa mfano kwake katika maisha; mbaya zaidi mtu yule maisha yake ni ya ajabu ajabu. Kwanini sasa aige maisha hayo? Ukifuatilia utakuta wanatabia zinazoendana au kukaribiana. Wana namna zinazoendana katika yale wayapendayo na yale wasiyoyapenda katika maisha yao. Na huu kwa hakika ni mfano uliohalisi, kwamba jaribu kuchunguza wale watu waliomarafiki. Utakuta kuna kitu wanashirikiana aidha kitabia na mwenendo mzima wa maisha.
Kumbe tambua kuwa kila mtu anabahati yake kuanzia leo. Sasa wewe utasema naishi hivi kwa maana hata fulani anaishi hivi na maisha yanaenda. Ila jua kila mmoja alizaliwa kwa mama yake pekee, si hivyo tu tena kila mmoja alizaliwa peke yake, anaishi peke yake, atakufa peke yake na mwisho atazikwa pekeyake. Kwa kujua hilo ndiyo maana kila mtu anakuja na bahati yake. Kwa hiyo, haya malimwengu yasikusumbue kabisa; kwa kuwa tumeyakuta. Kwani tumezaliwa tuli uchi na tutarudi vivyo hivyo.[2] Huyu rafiki yako, swahiba, shosti wote umewakuta tu. Kumbe huna sababu yoyote ya kumfanya mtu huyo awe kama mungu-mtu. Ndiyo maana ukiwa mtu wa kuchukua na kuiga kila kitu kama kilivyo (copy and paste) kwa mwingine unaweza kuishia kubaya. Maana huwezi yeye ameandikiwa nini na Mungu, maana yeye tunaambiwa alitujua tungali tumboni mwa mama zetu.[3] Ndo hiyo utashangaa mwenzako, licha ya maisha yake mabaya aliyokuwa anaishi ila dakika za mwishoni anamrudia Mungu; ila wewe isitokee hivyo. Kwa hiyo tujihadhari sana katika maisha yetu. Tujiepushe na kuiga kila kitu bali yale yaliymazuri basi tuyaige na kuyafuata. Lakini katika yale yanayoweza kutupotosha au kutupeleka katika njia isiyo sawa, ambayo inaweza kututenga naye Mungu; basi hatunabudi kuyatupilia mbali. Kwa maneno mengine hatunabudi kuachana nayo tena moja kwa moja.