Amri za Kanisa
Kuna jumla ya amri sita za Kanisa. “Amri hizi za
Kanisa zimepangwa katika fumo wa maisha ya maadili, zikifungamanishwa na
kulishwa na maisha ya Liturujia. Sheria hizi zilizowekwa wazi na mamlaka ya
kichungaji zina hali faradhi kwa lengo la kuwathibitishia waamini kiwango cha
chini kabisa cha lazima katika roho ya sala na juhudi ya maadili, katika kukua
katika mapendo kwa Mungu na jirani.”[1] Nazo ni zifuatazo kulingana na Misale ya
waumini:[2]
1.
Hudhuria Misa Takatifu Dominika na sikukuu
zilizoamriwa.
Inamtaka mwamini kutakatifuza siku
ya kumbukumbu ua fumbo la Ufufuko wa Bwana, lakini pia sikukuu kubwa za
kuheshimu mafumbo ya Bwana, ya Bikira Maria Mwenye heri, na ya Watakatifu.
Kwanza, kwa kushiriki adhimisho la Ekaristi ambamo jumuiya ya Kikristo inakusanyika,
na kupumzika na kuacha zile kazi na shughuli ambazo kwayo zingezuia
kutakatifuza siku hizo.[3]
Lakini pia mwamini apumzike kwa kuacha
kazi nzito.[4]
2.
Funga siku ya jumatano ya majivu; usile nyama siku ya
Ijumaa Kuu.
Ndugu
yangu unayesoma kitabu hiki, unapoongelea Jumatano ya Majivu huwezi kutupilia
mbali Kwaresima, maana Jumatano ya Majivu ndiyo mlanngo wa kutuingiza katika
Kwaresima. Kumbe hatuna Kwaresima pasipo Jumtano ya Majivu. Siku ya Jumatano ya
Majivu tunaanza rasmi kipindi cha Kwaresma ambacho kinadumu kwa muda wa siku
arobaini. Kwa nini siku arobaini? Waisraeli walikaa jangwani sku arobaini,
gharika kuu ilidumu siku arobaini, Yesu alifunga siku arobaini, kwaresma
inadumu siku arobaini. Miaka/siku arobaini katika Maandiko matakatifu inawakilisha
kipindi kamili cha mpito ambacho ndanimo jambo linaweza kufanyika na
likakamilika. Hivyo Kwaresma ni kipindi kamili cha mpito ambacho ndanimo
mapinduzi ya kiroho yanaweza kufanyika. Ni kipindi cha kufanya maandalizi ya
kuadhimisha sikukuu ya Pasaka. Na hivyo
kinaambatana na kupakwa majivu yatokanayo na matawi tuliyotumia Dominika ya
matawi; katika paji la uso kwa waamini lakini kwa Waklero kichwani. Katika
kipindi hiki mama Kanisa anatualika kufanya tathimini ya mahusiano yetu na
Mungu. Ni kipindi cha kufanya mapinduzi ya kiroho.Waamini tunahimizwa kwa
naamna ya pekee kuhudhuria liturjia ya leo.[5]
Majivu tutakayopakwa ni alama ya ukubali wetu kwamba sisi ni wadhambi, hatuna
thamani mbele ya Mungu na tunahitaji kufanya toba.
Katika
ulimwengu wa wayahudi majivu yalikuwa ni alama ya huzuni, masumbuko, uchungu au
uduni.[6]
Baadaye utamaduni huu wa kupakana majivu ulitumiwa na wakristo wa kwanza kama
alama ya toba. Mwaka 600 hivi, Gregory Mkuu aliifanya siku ya Jumatano ya
majivu kuwa siku ya kwanza ya Kwaresma na akaongeza urefu wa kipindi hiki cha
toba hadi siku arobaini. Miaka ya 800 hivi, baadhi ya makanisa yaliadhimisha
ibada ya Jumatano ya majivu kwaajili ya wadhambi waliokubuhu katika dhambi na
waliojulikana. Sasa pale walipoamua kufanya toba ndio walipakwa majivu. Hivi
wakati huu si wote walipakwa majivu ila tu wale walikuwa wadhambi waliojulikana
wazi, kama vile Malaya, wauaji, waasi n.k. Kuanzia karne ya 11, Kanisa
lilipanua ibada hii na kuwahusisha waamini wake wote na si wadhambi waliokubuhu
tu. Hatua za kuchukua ili tuweze kufanya vema mapinduzi ya kiroho, toba na
kubadilika. Tukubali kwamba sisi ni wadhambi. Tusipokubali kuwa sisi ni
wadhambi halafu hatutaona hitaji la kufanya toba na kubadilika. Ndio maana
tunapakwa majivu ikiwa ni alama ya kukubali kuwa sisi ni wadhambi hatuna
thamini mbele ya Mungu, na hivi tunahitaji kutubu. Kutumia misaada mbalimbali
ambayo itatusaidia kumrudia Mungu: Sala, kufunga na matendo ya huruma. Na hivyo
kwa kutambua tu wadhambi ndiyo maana tunapaswa kufunga siku hiyo ya Jumatano ya
majivu.
Lakini
pia usile nyama siku ya Ijumaa Kuu. Tukumbuke ndiyo siku Mkombozi wetu Yesu
Kristo anakufa msalabani. Na hivyo hatupaswi kula nyama kama waamini wenye
kutambua thamani ya wokovu wetu. Kwahiyo, ni siku ambayo waamini wanakuwa katika
huzuni, wakiomboleza juu ya kuondokewa na Mpendwa wao. Kama tujuavyo katika
hali ya maisha yetu ni kwamba nyama inatumika na kuthaminiwa kama chakula fulani
cha hali ya juu, yenye thamani na nzuri sana; ni katika uzuri huo watu wanaona
fahari na kuwafanya wafurahie. Mfano mzuri ni huu, ukitaka kuona au kusikia
sherehe fulani wanaisifia kuwa ilikuwa nzuri; wengi waseamao utasikia yaani
walijipanga kwelikweli: nyama ilikuwa ya kutosha kwa maana walichinjwa labda
ng’ombe watano (5) na kitakachofuata ni kinyaji, utasikia kulikuwa na pombe ya
kutosha kama ni ya kienyeji au bia au divai n.k. Kwa hiyo, hatunabudi kufunga
siku hiyo kula nyama.
3.
Ungama dhambi zako walu mara moja kila mwaka.
Pia sheria hii yahakikisha
maandalizi kwa ajili ya Ekaristi kwa kupokea Sakramenti ya Upatanisho.[7]
Hii inaonyesha mwendelezo wa kazi ya wongofu na msamaha wa Ubatizo.[8]
4.
Pokea Ekaristi Takatifu hasa wakati wa Paska.
Kama nilivyotangulia kusema, sheria
hizi za Kanisa kuwa inatoa walau kiwango cha chini. Kumbe amri hii yahakikisha
kiwango cha chini cha kupokea Mwili na Damu ya Bwana kuhusiana na sikukuu za
Pasaka, asili na kilele cha Liturujia ya Kikristo.[9]
Na hii inaenda sambamba na wale wanaoweza kushiriki Misa zaidi ya moja.
Waliowengi hawajui ya kuwa kama umemaliza Misa hii na ukampokea Yesu katika
maumbo ya mkate na divai, unapoenda Misa nyingine una haki ya kumpokea tena.
Siyo useme tu nimemaliza kumpokea Misa iliyopita na sasa sitaki au siwezi, wewe
mpokee labda kama unaona hufai pengine kiroho. Lakini kulingana na mazingira
unaruhusiwa kumpokea hata kama unajua kiroho ni mdhambi. Pengine ni kigangoni
na Padre amekuja kwa kuchelewa kwa sababu za kichungaji, basi usishindwe kwenda
kumpokea ilimradi tu ulikuwa umeshaweka nia ya kuungama kwanza. Na hivyo ukiwa
katika nia hiyo unaruhusiwa kukomonika, ila unuie kuwa mara baada ya kukomonika
basi unamtafuta Padre kwa maungamo. Ukifanya hivyo utakuwa hujatenda dhambi na
katika kumpokea Yesu maadam hujasitahilishwa basi inakuwa siyo kufuru na
unakuwa hujajitwalia hukumu yako.
5.
Saidia Kanisa Katoliki kwa zaka.
Ina maana ya kwamba waamini wana
wajibu na kazi ya kusaidia kutoa mahitaji ya Kanisa kila mmoja, kadiri ya uwezo
wake.[10]
Zaka hii inapaswa kutolewa fungu la kumi la kile unachojaliwa au ulichojaliwa.[11]
6.
Shika sheria Katoliki za ndoa.
Lakini kwanza tutambue kuwa ndoa ni
sakramenti kwa wakristo na hasa kwa wakatoliki. Ndoa ni agano kati ya mtu mume
na mtu mke. Ndoa ni aganao linalowafanya wanandoa kusihi pamoja kwa maisha yao
yote.[12]
Kwa kweli nakosa hata nguvu za kuongelea juu ya amri hii. Walio wengi naamini
ni mashahidi, ya kwamba amari hii haitendewi haki na wale wenye kuitendea haki.
Sina uhakika ni watu wangapi ambapo kwa uwazi kabisa tukiwauliza juu ya amri
hii kama wanaijua vilivyo; hususani wanandoa. Mama Kanisa katuwekea sheria
jumla mia moja na kumi na moja (111) za ndoa.[13] Sheria zenyewe hizi zimegawanyika katika
sehemu kumi (10) kwa kadiri ya Kitabu cha kanuni ya Kanisa Katoliki toleo la
pili la mwaka 1983.
a)
Mtazamo
wa kichungaji na nini kinatangulia maadhimisho ya ndoa (Pastoral care and what
must proced celebration of marriage)
b)
Vipigamizi
vya ndoa kwa ujumla (Diriment impediment in general)
c)
Vipingamizi
vya ndoa moja kwa moja (Diriment impediment specifically)
d)
Makubaliano
ya ndoa (Matrimonial consent)
e)
Nguvu
ya ndoa (Force of marriage)
f)
Ndoa
mchanganyiko (Mixed marriage)
g)
Kuadhimisha
ndoa wa siri (The secret celebration of marriage)
h)
Athari
za ndoa (Effects of marriage)
i)
Kuwatenganisha
wanandoa kwa muda (Simple separation of spouses)
j)
Kuhalalisha
ndoa ambayo haikuwepo (The convalidation of marriage).[14]
[1] KKK Na. 2041.
[2] Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania,
Misale ya Waamini, Toleo la Kumi, TMP Book Department, Tabora- Tanzania, 2008,
uk. 1077.
[3] Rej. MSK. Na. 1246- 1248.
[4] Rej. KKK Na. 2042.
[5] Rej. Katekisimu ndogo ya Katoliki
Jimbo la Iringa, Na .97, 100.
[6] Rej. Ayu 2: 8, 30: 19; Zab 102: 10.
[7] Ibid.
[8] Rej. MSK. Na. 989, 719.
[9] Rej. Sheria za Kanisa Katoliki, CIC
Na. 920, 708, 881.
[10] Rej. Sheria za Kanisa Katoliki, CIC
Na. 222, 1249-1251, 882, 25.
[12] Rej. Elias Nada, Karne ya Ishirini na Moja na Ndoa za Kikristo, Sayansi, Maisha ya
Familia na Ndoa, Chapa ya pili, Timia Printers, Moshi, 2015, uk. 25.
[13] Rej. Sheria za Kanisa Katoliki za
Ndoa, Mada ya saba Ndoa (CIC 1055-1165).
[14] The Code of the Canon Law, New
Revisedd English Translation, Harper Collins Publishers, Newsland, 1983,
237-258.
[15] Eze 18:23-28.
No comments:
Post a Comment