Tuesday, January 28, 2020

KIFO


 Sababu zinazoweza kupelekea Kifo[1]

Kila mmoja wetu amekwisha kutambua ya kuwa kifo ni lazima tukipitie. Kwa kuwa hata katika uumbaji (uhulushi) tunajua ya kwamba mwanadamu ni mwili na roho. Mara tu baada ya kutungwa kwa mimba, basi Mungu mwenyewe ndiye aiwekaye roho hiyo. Mwili daima unakufa, lakini roho kamwe haifi. Ndiyo maana mtu baada ya kufa mwili ule unaoza kwani umeumbwa kwa kitufaa (matter or material). Kwa lugha nyingine ni kwamba; ‘material body or things normally corruptible, hence decay’.[2] Kwani kupitia kuonja mauti, ndiyo njia pia itupasayo kufika kwa Baba. Huko ndipo tutaenda kuishi na kustarehe kwa umilele. Sasa kwa kuwa kifo ni matokeo ya dhambi ya asili waliyoifanya wazazi wetu wa kwanza yaani Adamu na Eva. Zifuatazo zinaweza zikawa sababu ambazo zinaweza kupelekea kifo, kwa kila mmoja wetu. Japo ni fumbo kwetu kama wanadamu kutambua tutakipitia kifo kwa njia ipi. Ila uhakika tulionao tu ni kwamba lazima kifo tukipitie.

1 Magonjwa

Kama tutambuavyo mapisi (historia) ya Adamu na Eva kule bustanini, ya kuwa waliishi vizuri na wanyama tena. Lakini baada ya kukosa utii, Mungu aliamua kuwafukuza bustanini na kuwapa mapigo kadhaa. Kama tutambuavyo ya kuwa hata dhahabu hujaribiwa kwa moto, ndivyo hivyo nasi tunakutana na magonjwa mbalimbali ili kuyafanya maisha yaende cha mikikimikiki. Kwa hiyo, maisha yetu kutokana na waandami (watangulizi) yaani wazazi wetu wa kwanza, nasi hatunabudi kuyapokea mahangaiko, mateso yatokanayo na maradhi. Kwani ardhi yote imelaaniwa kwa sababu wazazi wetu, vivyo hivyo nasi tunapatwa na yale aliyosema Mungu kama laana juu yetu.
Sasa katika maisha yetu tunaona na kushuhudia watu wengi wakifa kwa sababu mbalimbali za magonjwa. Na kinachosikitisha zaidi ni kwamba wakati huu watu wamekuwa wengi na magonjwa nayo yameongezeka sana. Kuna magonjwa ya aina mbalimbali ila zaidi ni ya kuambukizwa na yale yasiyoyambukizwa. Lakini yote katika yote unachelewa kupata huduma basi ugonjwa ukawa umeshamaliza au umeshatawala mwili kwa kiasi kikubwa basi hata matibabu unayowekupata yanaweza tu kukusaidia kusogeza siku au hata masaa. Magonjwa ambayo ni tishio sana kwetu mpaka sasa ni Mgandamizo wa damu (Presha), kisukari, ugonjwa wa moyo, saratani au kansa, UKIMWI pia malaria. Haya kwa kiasi kikubwa yamekuwa changamoto sana siku hizi. Mbaya zaidi yaliyomengi yanayoonekana kuwa kama tishio kwa kipindi hiki, mengi yanachangiwa na matumizi ya vyakula. Tunajikuta tumelalia kula vyakula vya kisasa (vyakula vinavyopita viwandani) zaidi kuliko vile vya asili. Vyakula vilivyojaa sana mafuta.
Tahadhari ni kwamba watu waanze kuwa na mazoea ya kupima na kuchunguza afya zao mara kwa mara ili kujua maendeleo ya afya zao. Hii isifanyike kwa ratiba bali iwe kila mara unapopata nafasi ya kufanya hivyo basi fanya. Kwani unapogundulika unatatizo fulani na ukawa tayari kufuata maelekezo ya Madaktari, aidha kwa kuacha kula aina fulani za vyakula au kwa kula aina fulani tu za vyakula basi utakuwa katika nafasi nzuri ya kuuweka mwili wako katika mazingira safi ya kupamabana na maradhi mengine ambayo yanaweza kujitokeza.
Lakini pia kuna maradhi mengine sisi wenyewe tumekuwa chanzo cha kuyasababisha. Kwa mfano kuna magonjwa ya mripuko ambayo unakuta chanzo chake kikuu ni kushindwa kutunza mazingira yetu salama. Hali tukitambua kuwa tukiyatunza mazingira hakika nayo pia yatatutunza. Kwa mfano kuna watu wanakufa kwa sababu ya mripuko wa ugonjwa wa Kipindupindu au Ebola. Sasa mtu watu hawa waathirika wanapokosa msaada wa huduma ya haraka lazima tuwapoteze, maana hamna namna. Kwa hiyo, tuwe makini na tutunze mazingira yetu nayo yatatutunza na kutuweka salama.

2 Ajali

Si kila ajali inatokea kwa sababu ya uzembe wa wale wenye dhamana ya kuongoza vyombo hivyo vya safari. Lakini zilizo nyingi chanzo kikubwa ni uzembe wa wahusika. Kuna aina mbalimbali za usafiri ukiwemo wa nchi kavu (Barabarani), majini pia angani. Sasa mara nyingi utakuta ni uzembe wa Dreva ama Nahodha ama Lubani kushindwa kuwa makini wakati anaongoza chombo. Na hii inatokana na kuwa na mawazo tawanyishi. Yaani mawazo yake muda fulani yanakuwa yametawanyika, badala ya kuwaza kile chombo anachoongoza anawaza yaliyo nje ya pale. Sasa hali hiyo inapoendelea inaweza kumfanya apoteze mwelekeo. Apotezapo mwelekeo tu, maana yake anaposhindwa kufuata vigezo na masharti ya uongozaji basi utasikia ajali imetokea.
Si hivyo tu, bali wakati mwingine inatokana na uchakavu wa vifaa au vimbo hivyo. Yaani unakuta ni chombo cha usafiri na kila siku au kila mara kiko safarini, kwa bahati mbaya uangalizi unapokuwa hafifu au mdogo. Sasa kama hamna uangalizi (kufanya service), kuna siku kinaweza kuwa kibovu na kwa kuwa hakina uangalizi wa mara kwa mara au kabla ya kuanza safari; basi mwisho wa siku kikiwa safarini na tatizo limeshakuwa kubwa utasikia kimepata ajali na watu kadhaa wamefariki dunia papo hapo na wengine kadhaa wamejeruhiwa. Kwa hiyo, kuwa na muda wa kuwa tunavihakiki ubora wake ni muhimu sana.
Mara nyingine pia mazingira ya hali ya hewa yanaweza kusababisha ajali. Kuna wakati hali ya hewa ndani ya maji inachafuka yaani unakuta mawimbi yameongezeka na chombo kiko safarini au chombo kiko angani na huko kinakutana na kani ya mvutano na hivyo kupelekea chombo hicho kupoteza mwelekeo. Hatimaye kinashindwa kumudu au kukabiliana na hali hiyo, basi kinabaki kuongozwa na hali ya hewa ya wakati huo. Na baadaye utasikia kimepata ajali. Kama tujuavyo Meli ya Mv. Bukoba ilivyozama tarehe 21-05-1996 na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 800.
Lakini pia sababu nyingine ya ajali inakuwa ni Dreva mwenyewe asiyejali mwendokasi. Mfano ulio hai ni huu, kuna aina tatu za Madreva; Dreva Kenge (huyu ni Dreva wa kukurupuka, pasipo kujali ubora wa chombo chake pia mwendokasi), Dreva Nyoka (huyu anaendesha kwa kupindapinda, yaani anaenda kwa kukatakata makona mfano anataka kumpita mwenzake shemu mbaya au isiyoruhusiwa na akiwa katika mwendokasi), na wa mwisho ni Dreva Kinyonga (huyu ni Dreva anayeendesha kwa usalama na anafuata kanuni zote za barabarani vizuri). Kumbe mwendokasi unapelekea wakati mwingi ajali, maana anapokutana na kona kali na yuko mwendokasi lazima limshinde kukata kona, mwisho wa siku gari litamshinda kumtawala na kuanguka au kupindukapinduka.
Ajali nyingine zinakuwa za mtu husika mwenyewe. Pengine ni fundi umeme. Sasa akiwa yuko juu ya nguzo akateleza na kuanguka, kwa bahati mbaya akaangukia sehemu mbaya. Kumbe inaweza kumpelekea katika kifo. Wakati mwingine watoto wanapenda kukwea juu ya miti yenye matunda misimu yake ikifika. Sasa inatokea wakati fulani akiwa amekwea anakanyaga tawi vibaya au tawi alilokanyaga bila kujua likawa limeshakauka. Mwisho wa siku anajikuta ameshashuka nalo chini. Na pengine mazingira ya pale chini yakawa hayako vizuri, basi anapoanguka vibaya basi inaweza kumpelekea katika kifo.

3 Vita

Kinyume cha vita ni amani. Kwa hiyo, kwa maneno mengine vita ni ukosefu wa amani. Kumbe vita inaambatana na utumiaji wa nguvu kupita kiasi (yaani silaha). Vita kwa yenyewe siyo kitu kizuri, kwani mara zote inaenda sambamba na umwagaji wa damu kwa watu wasio na hatia au wenye hatia. Licha ya kwamba katika maadili inaongelea katika sababu yenye haki, basi kwa haja ya hali ya kujihami n akujilinda basi itumike. Lakini katika yote, licha ya sababu inayotambulika hata kimaadili. Bado vita lazima ihusishe mauaji. Kwa mfano wa vita ya kwanza ya dunia mwaka 1918, pia tazama mauaji ya kimbari (Mauaji dhidi ya Wtutsi) kule Rwandwa kati ya 7-04 mpaka 15-07 mwaka 1994. Sasa takribani watu 500,000 mpaka 1,000,000 waliuawa. Kati yao asilimia 70 wakiwa Watutsi;[3] vita zote hizi zilihusisha mauaji ya watu wengi sana. Tusiende mbali sana hata  kwetu tukikumbuka vita ya Tanzania na Uganda (Vita vya Kagera) dhidi ya Idi Amin Dada iliyodumu kwa muda miezi sita, kuanzia mwaka 1978 mpaka 1979. Inasadikika takribani Askari wa Tanzania 373, Raia pia takribani 1500 na Askari 600 miongoni mwa 3000 wa Libya nao waliuawa.[4] Ilihusisha vifo vya watu wengi tu. Na katika hao wapo waliokuwa hawana hatia lakini wengine walikuwa ni wenye hatia.

4 Mamlaka

Katika nchi basi serikali imetoa dhamana kwa chombo fulani kushughulikia mambo kama hayo ya utoaji wa uhai. Kwa mfano nchi ya  Tanzania imetoa mamlaka katika vyombo viwili kwa wale wanobainika kuwa waharifu. Kuna chombo cha Mahakama, ambayo ndiyo inayotoa hukumu kwa watu wanaobainika kufanya makosa makubwa. Lakini utekelezaji wa agizo la mahakama unafanya na chombo cha Magereza. Kumbe, pale mtuhumiwa anapokuwa amehukumiwa kifo yaani kunyongwa na mahakama; ni jukumu la Magereza kuteke agizo hilo kwa mujibu wa mamlaka waliyonayo. Sasa utekelezaji wa mamlaka huo unapofanyika, basi hupelekea kifo kwa mtuhumiwa.

5 Kujitoa mhanga

Tumekuwa tukisikia mashambulio mbalimbali yanayotekelezwa na vikundi mbalimbali katika nchi fulani. Mashambulio haya ndiyo kusema kwa lugha nyingine ugaidi.  Utekelezaji wa kujitoa mhanga huu unawezakunywa na mtu mmoja, kwa kutumia silaha za miripuko; ambapo anatekeleza shambulio hilo la kujitoa mhanga akiwa katika mazingira ya kuzungukwa na watu wengi. Ni dhamiri ya kuwa kwa kutenda hivyo anajikuta kajiua na kuwaua wengine wengine. Kwa mfano tumekuwa tukisikia vikundi kama Alshababu kule Nchini Somalia, Boko haram kule Nchini Nigeria, Alkaida na vingine vingi. Ambavyo mara kadhaa vimekuwa vikiripotiwa kufanya mashambulizi ya kujitoa mhanga katika njia kadhaa. Kumbe kwa kitendo cha kujitoa mhanga tayari kinaambatana na mauaji ya watu.

6 Umri mkubwa

Hiki ni kifo cha asili (natural death). Kama tujuavyo kuwa uhai tumepewa na Mungu na unatoka kwa Mungu. Vivyo hivyo na maisha yetu yote yako kwa Mungu, kwani ndiye ajuaye ni katika umri gani basi tutapaswa kuyiacha dunia hii. Kwa hiyo, siyo wote walioandikiwa kufikia uzeeni, bali wale wachache. Sasa unapokutana na Mzee kabisa  aliyekula chumvi ya kutosha, yaani aliyefikia hatua ya kulelewa kama mtoto maana hajiwezi kwa lolote. Basi anapokufa tunaona kuwa ni kama haki yake, kwani umri wenyewe unaruhusu. Na watu wa namna hii mara nyingi huwa wanakufa wakiwa usingizini. Yaani kabla ya kulala mmeagana vizuri na hakuwa na tatizo au ugonjwa, ila asubuhi mnaamka kwenda kumjulia hali mnakuta ameshakufa. Kumbe umri unapokuwa wa kutosha basi mwisho wa siku zile seli nazo zinachoka mpaka kufikia hatua ya kutojiweza, hatimaye kupelekea kifo.

7 Majanga ya asili

Majanga ya asili wakati mwingine tunajitafutia vifo kupitia yenyewe aidha kwa kutokujua au kwa kujua. Kwa mfano mtu anaamua kwenda kujenga bondeni ambapo anajua mafuriko yakitokea hawezi kubaki salama, lakini anapoambiwa na kutahadharishwa ya kuwa anapaswa ahame ila yeye anabakia huko. Yakumkuta yakifika licha ya kuwa ni majanga ya asili lakini yeye kajiweka katika mazingira ya kukumbwa na matatizo. Kuna majanga ya kumbunga, tetemeko la ardhi, Tsunami, njaa, ukame pia miripuko ya Volkano. Haya yote ni baadhi ya majanga ya asili, hivyo yanapotokea kwa hakika hayawaachi watu salama. Kuna baadhi wanaenda nayo, yaani kifo kinawakabili. Hatuwezi kuyaepuka kwa kweli zaidi tunaaswa tu kuchukua tahadhari. Kwa mfano tetemeko la ardhi lililotokea mkoa wa Kagera mwaka 2017 lilisababisha maafa makubwa, watu kupoteza nyumba zao na mali zao pia wengine walipoteza maisha (walikufa).

8 Kifo cha maamuzi binafsi

kuna watu tumekuwa tukiwaona au kusikia au hata kushuhudia wakipoteza maisha aidha kwa kujitakia au kwa kutojitakia. Wale wanaojitakia ni kama wale wanaofikia hatua ya kukata tamaa ya kuishi, na mwisho wa siku wanaamua kuchukua uamuzi aliouchukua Yuda Iskalioti wa kujiua kwa kujinyonga. Sasa watu wa hivi mimi nawatazama katika mwono huo, ya kuwa wamejitakia. Lakini kuna wale wanakufa bila kujitakia. Kwa mfano unasikia mambo ya utoaji mimba ambao ni dhahiri ni kuuwa tu. Au mwingine anajifungua vizuri mtoto lakini mwisho wa siku anaamua kumtupa chooni au kichakani. Hicho nacho ni kifo cha mtu asiye na hatia na hakujitakia.



[1] Rej. Richard A. Kungi, Kupata nguvu Saa ya Majonzi, Maana na Uponyaji katika Kifo cha Umpendaye, FGD Tanzania Limited, Dar es salaam, 2018, uk. 4-12.
[2] Ludwig OTT, Fundamentals of Catholic Dogma, J. C. Bastible (ed), P. Lynch (trans.), Tan books and Publishers, Inc, Rockford, 1960, uk. 96-100.
[3] WIKIPEDIA- Rwanda genocide, https://en.m.wikipedia.org/wiki/Rwanda-genocide, retrived on 12/05/2019.

No comments: